Zimesalia siku kadhaa kumalizika mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani lakini katika siku za mfungo kumekuwepo na matukio ambayo kwa namna moja au nyingine yanaishangaza dunia kutokana na maeneo ambayo yanatokea matukio hayo kwa kuyahusisha na mwezi mtukufu.

Kama umekuwa mtu wa kufatilia habari zinazoendelea katika mataifa mengine utakumbuka kuwa wiki iliyopita ulitokea mlipuko katika kituo cha ndege Istanbul, Uturuki, mlipuko uliohusishwa na IS (Islamic State) na watu mbalimbali kujiuliza hawa IS ni Waislam au lah! maana sio jambo la kawaida kwa Muislam kufanya tukio hilo kwa mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Baada ya hilo, leo jumatatu ya Julai, 7 limeripotiwa tukio lingine la kutokea kwa mlipuko wa kujitoa muhanga katika mji wa Medina uliopo Saudi Arabia, mji ambao unatajwa kuwa mtukufu baada ya Macca kwa watu walio na imani ya Kiislam.

Mpaka sasa bado hazijaripotiwa taarifa za watu kupoteza maisha lakini tukio hilo linashangaza zaidi kutokana na sehemu ambayo mlipuko umetokea kwani ni karibu na Msikiti wa Mtume (Prophet Mosque) sehemu ambayo inatajwa kuzikwa Mtume Muhammad (SAW).

Katika hili linaweza kuumiza vichwa vya Waislam wengi na watu wote duniani ni nani anaweza kwenda kufanya tukio la kujitoa muhanga karibu na msikiti huo kutokana na heshima uliyonayo kwa watu walio na imani ya Kiislam.