Image result for tigo banner

LOWASSA aitikisa ARUSHA leo.

Mamia wajitokeza kumsikiliza Lowassa Arusha
Mgombea Urais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania kwa tiketi ya chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) Edward Lowassa ameendelea na kampeni kanda ya kaskazini ambapo leo amefanya mkutano mkubwa jijini Arusha kwenye viwanja vya shule ya Sekondari Sinoni.
Lowassa anayeungwa mkono kwa kiasi kikubwa na wasomi pamoja na vijana amewaambia wakazi wa mkoa wa Arusha kuwa ameamua kugombea Urais kwa kuwa anachukia umaskini.
Lowassa amesema kazi yake ya kupambana na umaskini ataianza kwa kutoa elimu bure mpaka chuo Kikuu.
“Nitaanza na elimu ili kuondoa hali ya umaskini. Vipaumbele vyangu vya kwanza elimu pili elimu tatu elimu. Ukimpa mtoto wako elimu umemsaidia kimaisha. Nimesema elimu kuanzia nursery hadi chuo kikuu bure,” amesema Lowassa.
“Wanasema haiwezekani mimi nasema inawezekana kabisa tuna fedha nyingi sana nchi hii kuanzia gesi mpaka madini na utalii. Hakuna mwanafunzi kulipa mchango wa aina yoyote. Nitazingatia maslahi ya mwalimu ili awe na moyo na kazi yake.”
Lowassa pia ameahidi kuboresha maisha ya wakulima kwa kupanua masoko ambapo atawaruhusu wakulima wauze mazao yao mahali yanapopatikana masoko bila vikwazo.
Wamachinga, bodaboda na mama ntilie nao hawakuachwa, ameahidi kuwawekea mazingira rafiki ya kufanya biashara zao.
“Mama ntilie na machinga watakuwa rafiki wa serikali yangu. Naahidi nikiingia ikulu baada ya wiki moja tu nitakuwa nimelidhughulikia tatizo lao la maeneo ya biashara. Nitaanzisha benki kwa ajili ya kupata mikopo ya riba nafuu.”
Lowassa pia ameahidi kujenga Hospitali za rufaa kila wilaya ambazo zitakuwa na vifaa vyote muhimu pamoja na dawa ili kuwaondolea wananchi adha ya ukosefu wa huduma muhimu za matibabu hasa vijijini.
Mamia wajitokeza kumsikiliza Lowassa Arusha
Aidha, katika mkutano huo, mwanasiasa mkongwe wa chama cha Mapinduzi(CCM) Kingunge Ngombale Mwiru ambaye alijitoa ndani ya chama hicho wiki iliyopita alipata nafasi ya kuzungumza na wananchi.
Kingunge amesema CCM imepoteza dira, haiwajali tena wananchi amesema hata kwenye kampeni zao wanatumia muda mwingi kuzungumzia watu badala ya kuzungumza masuala.
Amesema yeye ni mmoja wa watu wanopenda kuona mabadiliko katika Uchaguzi wa mwaka huu.
Kingunge amebainisha kuwa jitihada kubwa zilifanywa na vyama vya TANU na ASP kuboresha maisha ya wananchi hadi kuungana na kuunda CCM.
Amesema juhudi hizo zimeendelea kufanywa katika awamu zote za uongozi lakini amesema uongozi wa awamu ya nne umesaliti jitihada hizo.
Akitolea mfano ukuaji wa uchumi; Kingunge amesema wakati rais wa awamu ya tatu Benjamini Mkapa anaondoka madarakani uchumi ulikuwa unakua kwa asilimia 7%, Mkapa alichukua madaraka kutoka kwa Rais mstaafu Ali Hassani Mwinyi uchumi ukiwa unakua kwa asilimia 4%.
Amesema kwa mujibu wa takwimu za Serikali za hivi karibuni uchumi wa Taifa unaongezeka kwa kasi ya karibu asilimia 7, na kusema kuwa Taifa halijasonga mbele katika kipindi cha miaka 10 iliyopita.
Amesema CCM imechoka, imeishiwa pumzi ya kupambana na matatizo ya wananchi hivyo ni wakati muafaka kwa chama hicho kupumzishwa.
Kingunge amewataka wananchi kutofanya makosa tarehe 25 Oktoba kwa kufanya uamuzi sahihi wa kumchagua Edward Lowassa kuwa Rais wa Tanzania pamoja na wagombea wa nafasi mbalimbali kutoka vyama vinavyounda UKAWA.
Viongozi wengine waliohutubia katika mkutano huo ni Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Waziri Mkuu mstaafu awamu ya tatu, Fredrick Sumaye.
Akihutubia katika mkuano huo, Sumaye amesema kuwa chama cha Mapinduzi kimeharibu elimu pia kimeshindwa kuwapatia vijana ajira baada ya kuuwa viwanda.
Amebainisha kuwa Tanzania inahitaji rais muadilifu, awe mtumishi mwema,na awe kimbilio la watu.
Amesema mgombea wa CCM Dr John Magufuli hana sifa za uadilifu kwa kuwa wizara ya ujenzi aliyoiongoza kwa miaka mingi, kitengo cha mizani kina kashfa kubwa za rushwa.
Amesisitiza kuwa wizara hiyo inaongoza kwa rushwa.
Pia amemtuhumu Dr Magufuli kwa kununua meli ya miaka 30 kwa gharama ya meli mpya.
“Wizara ya ujenzi inaongoza kwa ufisadi,Je Magufuli ni mwadilifu?,” alihoji Sumaye.
“Ameshindwa kupambana na ufisadi wizarani kwake ataweza kwa nchi?”
“Lazima rais awe msikivu,je Magufuli ni msikivu?”
“Kigamboni aliwaambia watu wapige mbizi Maana yake wafe.”

No comments

Powered by Blogger.